• Breaking News

    ..

    ..

    Wednesday 31 August 2016

    MTAPOTEZA SANA MECHI MKIWATEGEMEA WASHAMBULIAJI TU, NI RAHISI KUSHINDA MKIWEKEZA KATIKA KIUNGO

    Na Baraka Mbolembole
    IMG_0203
    Mabingwa watetezi wa ligi kuu Tanzania Bara, Yanga SC imeanza msimu wa 2016/17 kwa ‘ushindi wa kuridhisha’ kufuatia kushinda 3-0 dhidi ya African Lyon siku ya Jumapili iliyopita. Nilitaraji hilo, Azam FC ilishinda 3-0 dhidi ya Majimaji FC, Tanzania Prisons ililazimishwa sare ya kufungana 1-1 nyumbani, Sokoine Stadium na timu ya Ruvu Shooting.
    Mtibwa Sugar ikicheza kwa mara ya pili Manungu Complex ilifanikiwa kupata ushindi wa kwanza mbele ya Ndanda FC. Matokeo mengine, Mwadui FC baada ya kupoteza game ya kwanza dhidi ya Toto Africans katika uwanja wa CCM Kirumba imefanikiwa kuondoka na pointi 3 katika game mbili za Mwanza kufuatia kuishinda 1-0 timu mpya kabisa katika ligi-Mbao FC.
    Kagera Sugar walikuwa wenyeji wa Stand United katika uwanja wa Kambarage, Shinyanga na kulazimishwa suluhu. Matokeo ya suluhu yalipatikana pia katika game JKT Ruvu na Simba siku ya Jumamosi. Mbeya City iliichapa 1-0 Toto Africans katika dimba la Kirumba.
    Kiujumla, ligi imeanza vizuri na ni timu moja tu iliyopoteza game zote hadi sasa (Ndanda, walifungwa 3-1 na Simba, 2-1 na Mtibwa). Hakuna timu iliyofanikiwa kupata ushindi wa asiliamia 100 zaidi ya Yanga ambao wamecheza mechi moja tu.
    NI LIGI NGUMU KWA WASHAMBULIAJI?
    Sidhani, japokuwa wiki ya kwanza ilizalisha magoli 8 katika game 7. Yanga imecheza mara moja tu lakini tayari wamefunga magoli matatu, Simba imefanikiwa kufunga magoli matatu katika game zao mbili walizokwisha cheza, Mtibwa imefunga magoli mawili katika game mbili sawa na Prisons, Ndanda, na Shooting.
    Timu iliyofunga magoli mengi hadi sasa ni Azam FC na mshambulizi na nahodha wa kikosi hicho, John Bocco amefanikiwa kufunga magoli matatu kati ya manne ya timu yake katika mechi mbili zilizopita. Mwadui, Mbao, Toto, City na Lyon zimefanikiwa kufunga goli mojamoja kila timu huku timu za Stand, Kagera, na JKT Ruvu zikiwa bado hazijafanikiwa kufunga goli lolote hadi sasa.
    Washambuliaji wa kati wa Yanga, Mrundi, Amis Tambwe, Mzimbabwe, Donald Ngoma ambao kiujumla walifunga magoli 38 msimu uliopita walitoka ‘kapa’ lakini bado washambuliaji-viungo wa pembeni, Deus Kaseke, mfungaji bora wa msimu wa 2014/15 Saimon Msuva na Juma Mahadhi wamefanikiwa kufunga katika game yao ya kwanza ya msimu.
    Rashid Mandawa ambaye alitamba msimu wa 2013/14 akiwa na Kagera Sugar, akachemka msimu uliopita akiwa Mwadui FC juzi alifunga katika ushindi wa timu yake mpya-Mtibwa ilipocheza na Ndanda.
    Washambuliaji wameanza msimu na kufunga lakini bado wachezaji wa idara ya ulinzi wanaweza kuwanyima nafasi za kufunga kwa wingi kama ilivyokuwa msimu uliopita. Ndanda ndiyo timu iliyoruhusu nyavu zake mara nyingi (magoli matano) lakini bado wamefunga mara mbili katika game mbili za mwanzo.
    Kuna timu hazijafunga hata goli moja. Stand, JKT Ruvu, lakini bado wako imara katika safu za ulinzi. Viungo kama Shaaban Kisiga (Shooting,) Mudathir Yahya (Azam FC,) Shiza Kichuya (Simba,) Wazir Junior (Toto,) Ditram Nchimbi (City) ni baadhi ya wachezaji wa nafasi ya kiungo ambao wameshaingia katika orodha ya wafungaji, ni dalili njema kwa ‘ma-mido’ kuzibeba timu zao msimu huu ikiwa washambuliaji watashindwa kufunga.
    Washambuliaji wameanza kwa spidi ya chini, sijui utawa msimu wa aina gani kwao, ila viungo wameanza na kasi sana, wakiongozwa na wafungaji watatu wa Yanga, ni dalili za kutawala msimu huu na wataendelea kufunga ikiwa watashindwa kutazamwa kwa jicho la 3.
    Mkicheza vizuri na kujaribu kufunga magoli muhimu kwa msaada ya viungo wenu wa kati, mnaweza kushinda mechi nyingi, lakini mkicheza kwa kuwekeza magoli yote kwa kutegemea washambuliaji, mtakwama.
    Mtapoteza sana mechi mkiwategemea washambuliaji tu, ni rahisi kushinda mkiwekeza katika kiungo.’ Wakati mwingine mechi zinakuwa ngumu kwa washambuliaji na lazima viungo wabebe majukumu ya kufunga mara kwa mara ili kupata matokeo.
    Kwa ukaribu zaidi, tafadhali unaweza ku-LIKE PAGE yangu #BSports Tanzania . Utapata Updates za michuano mbalimbali

    No comments:

    Post a Comment

    HABARI

    HABARI

    MICHEZO

    LOGO

    LOGO

    MAOJIANO

    BURUDANI