• Breaking News

    ..

    ..

    Friday, 2 December 2016

    TOENI LESENI ZA MAFUTA, GESI KWA WAKATI- PROF. MUHONGO




    Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amewataka wataalam kutoka  Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC)  kutoa leseni kwa wakati kwa makampuni  yanayojihusisha na shughuli za utafiti na uchimbaji wa  gesi na mafuta nchini.

    Profesa Muhongo aliyasema hayo jijini Dar es Salaam kwenye kikao cha majumuisho  kilichoshirikisha makampuni yanayojihusisha na shughuli za utafiti na uchimbaji  wa gesi na mafuta nchini, Shirika la Maendeleo ya Petroli Nchini (TPDC) pamoja na watendaji kutoka  Wizara  ya Nishati na Madini, Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na Mamlaka ya Udhibiti wa Shughuli za Mkondo wa Juu wa Mafuta (PURA). 

    Alisema kumekuwepo na  tabia ya ucheleweshaji wa uhuishaji wa leseni  za utafiti na uchimbaji wa gesi na mafuta kwa makampuni yanayoomba leseni  jambo linalokwamisha utendaji wa makampuni hayo.

    Katika  hatua nyingine, Profesa Muhongo aliyataka makampuni yanayofanya shughuli za utafiti na uchimbaji wa gesi na mafuta nchini  kutuma maombi ya kuhuisha leseni zao  miezi sita kabla ya muda wake kuisha.

    Alisema kuwa biashara ya gesi na mafuta duniani ina ushindani mkubwa na  kutaka kampuni  za mafuta na gesi kuongeza  kasi ya  utafiti na  watendaji kutoka TPDC na  Wizara  ya Nishati na Madini kuongeza  kasi ya utoaji wa leseni.

    Aliongeza kuwa mahitaji ya  gesi yanazidi kuwa makubwa nchini kutokana na gesi hiyo kuhitajika majumbani, kwenye  viwanda na  kuzalisha umeme hivyo makampuni hayo yanatakiwa kuhakikisha kuwa gesi  ya kutosha inayoendana na mahitaji halisi inapatikana.
    Alisisitiza kuwa ili  nchi ya  Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zenye kipato cha kati ifikapo mwaka 2025 nishati ya umeme wa uhakika inahitajika na kuongeza kuwa gesi ndiyo itakayochangia  katika uzalishaji wa umeme wa uhakika.

    Mkutano huu ulifanyika ukiwa ni moja ya utaratibu wa  Waziri Muhongo kukutana na kampuni zinazojishughulisha na utafiti na uchimbaji wa gesi na mafuta kila baada ya miezi mitatu kwa ajili ya kujadili maendeleo ya shughuli pamoja na changamoto zake.

    No comments:

    Post a Comment

    HABARI

    HABARI

    MICHEZO

    LOGO

    LOGO

    MAOJIANO

    BURUDANI