
Makamu Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein na Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF) Maalim Seif Sharif Hamad watafunga mikutano ya kampeni za uchaguzi mdogo wa ubunge wa Jimbo la Dimani unaotazamiwa kufanyika Jumapili.
Kwa mujibu wa taarifa zilizotolewa na Ofisi Makao Makuu ya CCM Kisiwandui Dk. Shein atafunga mikutano ya kampeni za kumnadi mgombea wa CCM Juma Ali Juma ambaye anapewa nafasi kubwa ya kuibuka na ushindi.

Katibu wa Kamati Maalumu ya Halmashauri Kuu ya CCM Zanzibar, Idara ya Itikadi na Uenezi Waride Bakari Jabu alisema kampeni hizo zitafikia tamani kwa Dk Shein kuhutubia mkutano wa mwisho wa kampeni.
Katika hatua nyingine Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif anatazamiwa kufunga mkutano wa kampeni za uchaguzi mjini Fumba Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Chama cha CUF katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Dimani kimemsimamisha mgombea wake Abdulrazak Khatib. Jumla ya vyama vya siasa 12 vinashiriki katika uchaguzi huo huku chama cha CCM na CUF vikionesha kuwepo mchuno mkali ambapo uchaguzi huo unafanyika kufuatia kifo cha aliyekuwa Mbunge wa jimbo hilo Hafidh Ali Tahir (CCM) aliyefariki akiwa katika mkutano wa Bunge mjini Dodoma mwaka jana.
Mapema jana Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) ilisisitiza kwamba watu watakaopiga kura ni wale ambao wamesajiliwa katika daftari la kudumu la wapiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba mwaka 2015.
No comments:
Post a Comment