Na Zawadi Msalla-WHUSM
Serikali imeahidi kuweka misingi
madhubuti ya kukuza lugha ya Kiswahili kwa kuhakikisha lugha hiyo
inatumika katika ngazi mbalimbali ikiwemo kufundishia katika taasisi za
kielimu, Mahakamani na Bunge.
Hayo yameelezwa na Waziri wa
Habari,Utamaduni,Sanaa na Michezo Mhe. Harrison Mwakyembe wakati wa
maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 60 ya kuzaliwa kwa Idhaa ya Kiswahili
BBC yaliyofanyika katika ukumbi wa Kilimanjaro-Hyatt Regency jana
Jijini Dar es Salaam.
Mhe. Mwakyembe ameeleza kuwa
Wizara yake ipo katika hatua za ukamilishaji wa kuundwa kwa sera mpya ya
Lugha ambayo itasimamia matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili na
kufanya matumizi ya lugha hiyo kukuwa katika ukanda wa Afrika Mashariki
na Afrika kwa ujumla.
“Serikali imejipanga kukifanya
kiswahili kuwa kati ya lugha tatu bora duniani,kwa sasa ni miongoni mwa
Lugha 10 maarufu kati ya Lugha 6000 na Lugha ya pili kutumika barani
Afrika” alieleza Waziri Mwakyembe.
Aliongeza kwa kueleza kuwa
uzinduzi wa Kamusi Kuu ya Kiswahili utachangia kwa kiasi kikubwa ukuaji
wa lugha hiyo adhimu huku Serikali ikihakikisha Kamusi hiyo inasambazwa
katika maeneo yote muhimu zikiwemo ofisi zote za Balozi za Tanzania
nje ya nchi, Taasisi za Elimu kuanzia ngazi za awali hadi za juu na
mahakamani .
Vilevile Mhe. Mwakyembe
amewapongeza wafanyakazi na uongozi wa Idhaa ya Kiswahili BBC kwa kuwa
mstari wa mbele katika kuhakikisha Lugha ya Kiswahili inatumika katika
matangazo yao na kukifanya kusikiwa dunia kote.
Aidha Waziri Mwakyembe alitoa
wito kwa watanzania wote kukipenda na kukienzi Kiswahili kwani ndiyo
kitu pekee kinachoweza kumtambulisha kila mtanzania mahali popote pale
duniani
No comments:
Post a Comment