Leo tarehe 30-8-2017 Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo Ndg. John L.Kayombo kwa kushirikiana na Madiwani wakiongozwa na Mstahiki Meya Boniface Jacob,,pamoja na maofisa wa TANROADS,Mkandarasi wa mradi wa Interchange-CCI-CCE,Jeshi la polisi,wenyeviti wa mtaa na watendaji wa kata za Makuburi,Sinza na Ubungo wamekutana na wanyabiashara maarufu kwa jina la Machinga na mama lishe ambao wanafanya biashara zao pembezoni mwa barabara ya Morogoro Road makutano na Mandela road Ubungo mataa sehemu ambayo Mradi wa barabara za juu (Interchange) unatarajia kuanza kujengwa.
Lengo la Mkutano huo lilikuwa ni kuongea na wafanya biashara hao kuwataka kuondoka katika eneo hilo ili kupisha ujenzi wa Barabara hizo za juu zinazotarajiwa kuanza kujengwa hivi karibuni ambazo zitarahisha usafiri na kuondoa kero za foleni ambazo zimedumu kwa muda mrefu.
Uongozi huo umeelekeza wamachinga hao na mama lishe eneo la kwenda ambapo umewaahidi kuwapeleka katika eneo la mawasliano Simu 2000 na kupatiwa sehemu za kufanya biashara zao katika soko hilo kwa utaratibu maalum.Na wale watakaoona wanaweza kwenda sehemu nyingine ambayo si eneo la mradi wamepewa fursa hiyo pia.
Akiongea katika mkutano huo Mstahiki Meya wa Mnispaa ya Ubungo amewasihi wamachinga hao kuondoka wenyewe pasipo kutumia nguvu yani kwa amani bila kutumika kwa nguvu ya jeshi la polisi kwa kuwa mradi huo ukitekelezwa unawanufaisha wananchi wote wa Ubungo na Taifa kwa Ujumla.
Nae Mkurugenzi akisisitiza katika hilo amesema ili mkandarasi aendelee na kazi anahitaji eneo husika kuwa wazi ili waweze kufanya kazi kwa ufanisi., alisema ninyi ni moja ya wananchi watakaonufaika na mradi huu hivyo kwa pamoja tunatakiwa kutoa ushirikiano ili kumrahisishia Mkandarasi aweze kuanza kazi hii ya ujenzi mara moja kwa kuacha eneo la mradi wazi,utaratibu umewekwa wa jinsi ya kupata eneo mtakalohamia ili muendelee kufanya biashara SIM2000.
Pamoja na kupewa maelezo hayo wamachinga walipata nafasi ya kuonyeshwa mipaka ya eneo la mradi ambalo linatakiwa liwe wazi kwa ajili ya ujenzi kwa kuenyeshwa alama zilizowekwa.Pia walipata nafasi ya kujibiwa maswali yao mbalimbali katika mkutano huo.
Wamachinga hao walipewa nafasi ya kuchagua wapewe siku ngapi za kujipanga kuhama eneo hilo ambapo wamesema siku tatu kuanzia leo zitawatosha kujipanga kuhama,pamoja na hilo mama lishe wa eneo hilo wamepewa nafasi ya kuendelea kuwapikia mafundi watakaokuwa wanajenga au kufanya vibarua katika ujenzi huo kwa utaratibu maalum watakaopewa pia na wengine watakaotaka kupata nafasi ya vibarua katika ujenzi fursa hiyo pia wataipata kwa kufuata utaratibu.
Utekelezaji wa Mradi wa Barabara za Juu katika eneo la Ubungo Mataa ni Muendelezo wa Miradi ya Barabara za Juu (Interchange) katika jiji la Dar es Salaam ambayo serikali ya awamu ya Tano chini ya Uongozi wa Rais John Pombe Magufuli amedhamiria kuitekeleza ili kurahisisha usafiri na kisha kurahisisha shughuli za uchumi kwa ujumla.
IMETOLEWA NA KITENGO CHA HABARI NA UHUSIANO UMC
No comments:
Post a Comment