Serikali ya China imeipatia Tanzania msaada wa Shilingi bilioni 29.4
kwa ajili ya kusaidia sekta ya elimu ya ufundi stadi, utalii wa
kijiolojia na kukarabati wa Uwanja wa Taifa Jijini Dar es Salaam.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango, Bw. Doto James (wa
pili kulia) na Kaimu Balozi wa China Nchini Tanzania, Mhe. Gou Haodong
(wa tatu kushoto) wakisaini makubaliano ya msaada wa Sh. bilioni 29.4
kwa ajili ya miradi ya Ujenzi wa Chuo cha VETA Mkoani Kagera, Utalii wa
Kijilojia na Ukarabati wa Uwanja wa Taifa, katika ukumbi wa Wizara ya
Fedha na Mipango Jijini Dar es Salaam. Picha na Kitengo cha Mawasiliano
Serikali Wizara ya Fedha na Mipango
Makubaliano ya msaada huo yametiwa saini Jijini Dar es Salaam na
Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Doto James, kwa niaba ya
Serikali, na Kaimu Balozi wa China hapa nchini, Mhe. Gou Haodong.
Bw. Doto James alisema kuwa kiasi cha Shilingi bilioni 22.4 cha
msaada huo kitatumika kujenga Chuo cha Ufundi Stadi-VETA wilayani Ngara
mkoani Kagera, ambacho kitakapo kamilika kitadahili zaidi ya wanafunzi
400.
“Fedha hizo zitatumika kujenga vyumba 19 vya madarasa, ujenzi wa
karakana 9 za kutolea mafunzo ya elektroniki, ufundi bomba, useremala,
ufundi uashi na upakaji rangi” alisema Bw. James
Alieleza kuwa kiasi hicho pia kitatumika kujenga majengo ya utawala,
mabweni, nyumba za walimu na miundombinu mingine itakayosaidia kuboresha
mazingira ya kujifunzia na kufundishia kwenye chuo hicho.
“Tunaamini kwamba msaada huo utakuwa sehemu ya kusaidia jitihada za
Serikali za kujenga uwezo wa wataalamu wake watakaochangia kukuza sekta
ya uzalishaji na hatimaye kutatua changamoto ya ukosefu wa ajira kwa
vijana nchini” alisema Bw. James
Katibu Mkuu huyo wa Wizara ya Fedha na Mipango Bw. Doto James
alibainisha kuwa katika makubaliano ya msaada huo, Jamhuri ya watu wa
China, itatoa kiasi cha shilingi bilioni 6.7 kwa ajili ya kuukarabati
Uwanja wa Taifa wa Michezo wa Dar es Salaam.
“Katika makubaliano yetu ya msaada wa kuendeleza Uwanja wa Taifa
wenye uwezo wa kuingiza watu 60,000, China itatoa msaada wa kiufundi na
vifaa vya kisasa vya michezo na utaalamu katika usimamizi na ukarabati
wa uwanja,” alifafanua Bw. James
Bw. Doto James alisema kuwa kiasi kingine cha shilingi milioni 300
kitatumika kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu wa kuanzishwa kwa aina
mpya ya utalii ujulikanao kama utalii wa kijiolojia “Geopark Project”
katika Hifadhi ya Taifa Ngorongoro, mkoani Arusha.
Alisema lengo la utafiti huo ni kuhakikisha kuwa Tanzania inanufaika
na maajabu mbalimbali ya kitalii yaliyopo nchini ambayo hayajatumika
kikamilifu kuvutia watalii watakaoongeza pato la Taifa
“Tanzania ina kila sababu ya kujifunza kutoka katika Hifadhi ya
Kimataifa ya Jiolojia ya Jiaozuo ya Yuntaishan ya China, iliyoanzishwa
mwaka 2000 ambayo inaongeza asilimia 37.2 ya watalii kila mwaka na
huchangia asilimia 12 ya pato la Taifa la nchi hiyo” aliongeza Bw. Doto
James.
Aliishukuru China kwa ushirikiano wake wa dhati na Tanzania tangu
miaka ya 1960 na kwamba mpaka sasa nchi hiyo imeendelea kuipiga jeki
Serikali katika ujenzi wa miradi mbalimbali ukiwemo upanuzi wa Chuo cha
Polisi Moshi, Ujenzi wa Maktaba mpya katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
na ujenzi wa Ofisi za Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika
Mashariki.
..
Saturday 30 September 2017
Home
Unlabelled
China yaipatia Tanzania msaada wa fedha kusaidia sekta ya elimu
No comments:
Post a Comment