• Breaking News

    ..

    ..

    Thursday 22 March 2018

    MPANGO WA MAJI SASA SAFI

    SERIKALI Mkoani Dar es Salaam, imesema inamatumaini makubwa ya kuwapatia  wakazi wake huduma ya maji kwa asilimia 95 ifikapo mwaka 2010 na asilimia 100 ifikapo mwaka 2025.

    Pia,  imesema kwa kushirikiana na Mamlaka zake za Majisafi na Majitaka (DAWASA na Dawasco) imejizatiti kikamilifu  kukabiliana na changamoto ya uondoaji wa majitaka ambapo kwa sasa ni asilimia 10 tu ya wananchi mkoani humo wanapata huduma hiyo.

    Akizindua ujenzi wa  mradi wa kuchakata majitaka unaojengwa katika Kata ya Mburahati, kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Mkuu wa Wilaya ya Ubungo,   Kisare Makori, alisema sera ya serikali  ni kuwafikishia huduma ya maji wananchi wake wote mkoani humo.

    Makori ambaye pia  alikuwa akihutubia katika kilele cha Maadhimisho ya Wiki ya Maji, mkoani humo, alisema, matumaini hayo yanatokana na  miradi mikubwa iliyokamilika na mipango inayoendelea  kutekelezwa na serikali  kupitia DAWASA na DAWASCO na Ofidi ya Mkuu wa Mkoa.

    “Kukamilika kwa  mradi mkubwa wa Ruvu Chini ambao  umeongeza upatikanaji  wa maji kutoka lita milioni 182 kwa siku  na kufikia lita milioni 270.

    Kukamilika kwa mradi huu kutaongeza  upatikanaji wa maji katika  maeneo ya Bagamoyo,Tegeta, Mbweni, Kinondoni, Chuo Kikuu, Kunduchi, Kawe, Mikocheni na maeneo ya katikati ya jiji,”alisema Makori.

    Pia, kukamilika kwa mradi mkubwa wa Ruvu Juu ambao alisema umeongeza  upatikanaji wa maji kutoka lita milioni 82 kwa siku na kufikia lita milionui 196 kwa siku.
    “Kumeongeza upatikanaji wa maji katika maeneo ya Kibaha, Kibamba, Mbezi, Kimara, Ubungo na Tabata,”alifafanua.

    Makori alisema kukamilika kwa visima 20 vya Kimbiji na Mpera vitaongeza  upatikanaji  wa  huduma ya maji kwa lita milioni 250 kwa siku maeneo yatakayohudumiwa na Wilaya ya Kigamboni, Temeke na baadhi ya maeneo ya wilaya ya Ilala.

    “Kukamilika kwa  miradi  ya visima10 vya mpango wa maendeo  ya sekta ya maji  ambapo visima tisa vilivyojengwa na manispaa vinahudumia watu zaidi ya 300,000,”alisema.

    Alisema hadi sasa  kumekuwa na ongezeko kubwa la wateja waliounganishiwa huduma ya maji kutoka 123,00 mpaka 268,000.

    Kuhusu  suala la mfumo wa majitaka, Makori, alisema, kukamilika kwa ujenzi wa miradi  midogo ya kusafisha majitaka  katika kata ya Toangoma na Mburahati itasaidia kwa kiasi kikubwa katika uondoaji wa majitaka katika makazi ya watu .

    “Kwa sasa ni asilimia 10 tu ya wakazi ndiyo wanapata  huduma ya kuondolewa majitaka lakini  serikali kwa kuishirkiana na DAWASA na Dawasco, pamoja na wadau  ipo katika hatua za utekelezaji miradi mikubwa,”alisema Makori.

    Alitaja mradi wa mfumo wa uondoaji majitaka  kwa wakazi wa mkoa wa Dar es Salaam, ambao utajengwa katika eneo la Jwangani  utakaokuwa na uwezo wa kusafisha lita za ujazo 200,000 kwa siku.

    “Mradi wa Kurasini utakuwa unasafisha lita 11,000 kwa siku, Mbezi Beach utasafisha lita za ujazo 16,000,”alisema.

    Aliongeza; ‘Mradi huu utahusu upanuzi  wa mfumo wa majitaka maeneo ya katikati ya jiji, ujenzi wa mfumo mpya Ilala , Ubungo na Kinondoni,”

    Alisema mradi wa maji na usafi wa mazingira unaofadhiliwa  kupitia program ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP II) utahusu  ujenzi wa mifumo 50 ya kukusanya na kusafisha majitaka  na ujenzi wa vyoo vya kisasa na utatekelezwa katika kipindi cha miaka mitano.
    Mhandisi wa mradi wa uchakataji maji taka Mburahati,  MOdekai Sanga alisema utakuwa na uwezo wa kuhudumia  wananchi  40,000 na utagharimu sh.milioni 95.

    No comments:

    Post a Comment

    HABARI

    HABARI

    MICHEZO

    LOGO

    LOGO

    MAOJIANO

    BURUDANI